Na pambe za taarabPambezataarab@gmail.com
Muziki wa taarabu una asili na fasili yake katika watu wa pwani na visiwani na maeneo ya mwambao wa Afrika Mashariki.
Umeathirika kwa kiasi kikubwa na muziki wa Mashariki ya Kati, India na kaswida za Kiislamu.
Sifa
moja kubwa ya muziki wa taarabu tofauti na wengi wanavyofikiri sio
maneno na mpangilio wake, bali ala za muziki huo na mipangilio yake na
ule ufundi wa kila mwanataarabu kuwa bingwa au stadi katika kupiga
chombo fulani. Taarabu isipokuwa na ala hizi sio taarabu ni igizo tu
kwa kiasi fulani la kitu kama taarabu. Taarab kwa kawaida ni kitulizo
cha fikra ndani ya nyumba na katika hadhara isiyoshawishiwa na usasa na
umagharibi kiasi cha kupuuza maadili na mila za wahusika.
Ala za
taarabu ni nyingi na swahiba wangu El-hatibu rajabu ambaye sio tu shabiki wa
taarabu bali ni mtunzi pia wa nyimbo za taarab anaweza baadaye kunipokea
hapa na kuelezea zaidi kwanini tunastahili kuwekeza kwenye taarab
asilia kama eneo la utamaduni linalostahili kuhifadhiwa na kuenziwa.
Taarabu
kama walivyoiendelza kina Siti binti Sadi, Bi Kidude, Juma Bhalo na
kina Sheikh Ilyas, Machapurala bila kuwasahau mamia ya wanawake na
wanaume wa Kizanzibar na Kimrima waliochangia maendeleo ya tasnia hii
adimu lakini iliyo na sifa ya kuwa sehemu muhimu ya utamaduni wa
mwambao ya Pwani ya Afrika Mashariki na usiostahili kuachiwa kupotea.
Taarabu
ni muziki wa enzi na enzi. Ni sehemu ya utamaduni endelevu na hususan
katika mikoa ya pwani ya Afrika Mashariki. Taarab ni ustaarabu,
utaratibu, upole na uungwana. Taarabu ni kitulizo cha mawazo na gundi
ya kuunganisha familia kama sio ukoo mzima. Sifa ambayo si mipasho, sio
rusha roho sio mnanda unayo.
Taarab kiasili sio muziki wa
kucheza bali wa kutazama, kusikiliza, kutafakari na kutunza. Huu ni
muziki uliokuwa ukisikilizwa na watu wenye fikira, busara na hekima
kuwapa muda wa kuwaza na kuwazua juu ya hili au lile. Muziki wa
kupayuka, kujiona, mashauzi, kusemana, kutukanana, kuumbuana na wenye
nyimbo ambazo hazina staha, usiri wala taadibu ya kuimbwa katika mafumbo
hauwezi kuitwa taarab.
Ni muziki ambao kwa kawaida una ala
takriban ya ishirini. Na kwa wapenzi halisi wa taarabu hufuatilia
upigaji wa kila ala na ufundi au ugwiji wa yule anayetumia ala husika.
Aidha, mashairi ya taarab hayaangalii tu mlingano wa vina na mizani bali
maudhui na mantiki ya kile kilichomo tena kikiwa kwenye mafumbo kuweza
kusomeka vyema na wanaosikiliza wimbo husika.
Ni muziki ambao
hutungwa kwa mafumbo na kwa namna ambayo hauzuii familia nzima, yaani,
babu, bibi,baba,mama, kaka na dada wote kujumuika kwa pamoja bila
kutokea chochote ambacho kinaweza kuwafanya washindwe kuzungumza au
kutazamana. Taarab kiasili uliunga pamoja familia za wakazi wa mji
husika. Tofauti na hiyo inayoitwa 'modern taarab' au 'taradance' ambayo kwa kiasi
kikubwa inazivunja familia katika kila mji na kijiji.
Siti bint Saad (1928) ndiye nyota wa kwanza wa taarab
ambaye
kwa mara ya kwanza badala ya kuimba kwa Kiarabu aliimba kwa Kiswahili.
Alifyatua mamia ya santuri za nyimbo India na wapenda muziki wa enzi
hizo hakuna aliyekosa wimbo wake nyumbani.
Muziki wa taarab asili
hauna tofauti na 'Classical Music' wa Ulaya au 'Country Music' wa
Marekani. Miziki hiyo ilikuwepo, imekuwepo na itakuwepo bila kubadilika
wala kuitwa kwa jina jingine wala kupigwa kwa namna nyingine tofauti na
ilivyokuwa, ilivyo sasa na itakavyokuwa kesho.
Ni sehemu ya kudumu ya utamduni wa watu na sio kitu cha kupita na kusahaulika.
Aina
hizo za miziki pamoja na kuzuka kwa miziki ya kila aina Ulaya na
Marekani bado inatambulika kwa nembo na jina lake. Country ni country na
classical ni classical. Hapajakuwepo muziki mwingine uliopewa umodern
kuhusiana na miziki hii, hakuna kitu kama modern country au modern
classic.
Rouget katika Music and Trance anafafanua kwamba neno
taarab linatokana na neno la kiarabu 'tariba' likiwa na maana ya hisia
za kusisimka, kudhihirisha au kutaka kufanya kitu fulani kama vile
kuimba au kucheza taarab.
Taarab asili ilingia kwanza hapa Afrika
Mashariki kupitia Zanzibar kunako miaka ya 1870. Aliileta Sultan Seyyid
Barghash ambaye alileta kikundi cha wanamzuki toka Misri kukaa kwenye
jumba lake la Kifalme.
Tofauti na viongozi wetu wa leo, Barghash
aliwapeleka Wazanzibari kadhaa wakiongozwa na IbrahimMohammed kwenda
kusomea muzki nchini Misri nao waliporudi waliunda kikundi cha kwanza
pengine cha taarabu Afrika Mashariki kilichoitwa Zanzibar Taarab
Orchestra.
Kunako 1905 kikundi cha pili cha taarabu kilizaliwa
huko huko Unguja kikiitwa Ikwhani Safaa Musical Club. Kikundi hicho
kipo hadi wa leo, lakini kama vilivyo vikundi vingine vya taarab 'hasa'
havina msaada wowote wa maana toka kwa yeyote yule, kwani inavyoelekea
wengi pamoja na viongozi wa serikali wametekwa na rusharoho na mipasho.
Taarab asili haistahili kuonekana kama ni taarab tu. Ni zaidi
ya taarab. Hii ni hazina ya utamaduni katika mwambao wa Afrika Mashariki
kuanzisa Lamu hadi Kilwa na Sofala.
Kama jitihada
zinavyofanyika kukarabati na kutunza maeneo kama vile Mji Mkongwe
Zanzibar, Bagamoyo na Kilwa ili iendelee kuwepo basi upo umuhimu pia wa
wanaohusika katika serikali zetu kuhakikisha kuwa muziki wa taarab
asili na wanamuziki wake wanakumbukwa na kuenziwa na kisha kizazi kipya
kinajengwa ili kuendeleza muziki huu kwa faida ya vizazi vijavyo. Kwa
maana, ukweli ni kwamba taarab asili ikipotea ndio utakuwa mwisho wa
taarab hapa Afrika Mashariki.
Kwanini tuhifadhi taarab asilia?
Kwa
bahati mbaya wengi tumezoea kuchukulia vitu kama ardhi, fedha, nyumba,
magari kuwa ndio rasilimali tu. Lakini muziki wa kiasili nao ni
rasilimali muhimu kimaendeleo na kisaikolojia. Bila urithi wa namna hii
tutakuwa ni taifa lipolipo tu ambalo si jambo zuri.
Pamoja na
mambo mengine kuifufua, kuitunza na kuiendeleza taarab asili ni jambo
lenye faida kadhaa ikiwemo kuendeleza mila na utamaduni wetu; kuzileta
familia pamoja mara kwa mara; kujenga maadili bora katika jamii; kuwa na
muziki usioendana kinyume na maadili ya dini; kukuza na kuendeleza
ushairi na Kiswahili; kuwa kivutio kwa wageni wa leo na kesho
na kuzienzi na kuendeleza ala asili za muziki na upigaji wake.
Miziki inayojiita modern taarab iitwe kwa
majina yao yanayostahili kama ni kiduku basi kiduku, kama ni rusha roho
basi rusha roho fulani, kama ni mipasho basi ni mipasho na kama ni
mnanda uitwe mnanda
na miziki hii isiruhusiwe kutumia mgongo wa taarab kujijenga isipostahili.
Nikiri
kuwa nilitaka sana nitembelee Lamu, Malindi, Mombasa, Tanga na Zanzibar
kuzungumza na wakereketwa wenzangu wa taarabu asili kabla ya kuandika
makala haya lakini haikuwezekana. Ninaamini, hata hivyo kupitia makala
haya ujumbe unaweza kufika kwa kiasi fulani.
Ninawashauri
wanaharakati wa kulinda na kuendeleza utamaduni wetu kuangalia uwezekano
wa haya yafuatayo: Kusaidia juhudi binafsi zilizopo za kufufua na
kuendeleza vikundi vya taarabu kupitia vilabu na vyuo vya upigaji ala
za asili za taarab (mathalani juhudi za Bi Hamdani, Zanzibar) ;
Kushirikiana na UNESCO kuhifadhi taarab asili kwa kutumia TEKNOHAMA;
Kuwatafuta
wanataarab asil waliko na kuwaunganisha ili kuufufua na kuchochea
kuwepo kwa muziki huo kiasili na kuongeza vionjo viwili vitatu vya
kuvutia familia zaidi kuliko mtu mmoja mmoja.
Aidha, kusaidia
vikundi vilivyopo lakini havina ala za kutosha za muziki toka Misri na
Uarabuni; kuenzi Ushairi katika vyombo vya habari kukuza vipaji vya
washairi chipukizi na
kuchukulia Taarab asili kama urithi usiostahili kupotea kwa msaada wa UNESCO na wapenda utamaduni wetu wengineo.
Baada ya Watanzania kugeuka wavivu wa kila kitu ikiwemo kupiga ala za
muziki na kutaka mteremko katika kila jambo wale waliozuka na mitindo
inayotumia mashairi au tungo zenye vina na mizani au isivyo hivyo
wakaona urahisi ni kuita miziki yao 'modern taarab' au 'taradance'. Miziki hiyo
ninakaata sio taarabu bali inastahili kuitwa mipasho, kiduku, rusha na
roho au mnanda na vitu kama hivyo lakini sio kamwe taarab.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni