TANGAZA NASI

Breaking

Jumapili, 23 Agosti 2015

OMARY TEGO:- NDOTO YANGU ILIKUWA KUWA MWANASOKA BORA NA SIO MUIMBAJI WA TAARAB, LAKINI.........

NA KAIS MUSSA KAIS


OMARY TEGO "THE SPECIAL ONE".

                 Alianza kupenda soka akiwa kijana mdogo, ndoto zake za awali zilikuwa kucheza soka, baadaye zikageuka na kujikuta akimbo taarabu. Wakati huo, Tego alikuwa na mazoea ya kufuatana na baba yake kwenye mazoezi na maonyesho ya kundi lililowahi kutamba la muziki wa taarab asilia la African Musical Club. Tego anasema alilazimika kubadili mipango yake kutokana na kuvutiwa na aliyekuwa muimbaji nyota wa taarab nchini na katika ukanda nzima wa Afrika Mashariki na Kati, marehemu Issa Matona aliyekuwa akiliimbia kundi hilo pamoja na baba yake.

Anasema, "kwa kweli sikuwaza kuja kuwa mwanamuziki, ndoto zangu zilikuwa ni kuwa mchezaji wa soka, lakini kumshuhudia na kumsikia marehemu Issa Matona nilijikuta nabadilisha mawazo na kuanza kujifunza muziki kupitia kundi hilo la Africa Musical Club mwaka 1995," Tego anasema kabla ya kupenda muziki kupitia kwa baba yake, aliyekuwa muimbaji na kiongozi wa kundi la African, alikuwa 'kichaa' wa soka, akianza kucheza timu ya Santos ya Mtoni alipokuwa akiidakia kabla ya kucheza nafasi za mbele baadaye.

Anasema, "nilianza kucheza soka tangu nikiwa Shule ya Msingi Sokoine na timu yangu ya mtaani ilikuwa ni Santos niliyokuwa nashiriki nayo kwenye michuano ya Yosso kama golikipa, kabla ya kuvutwa na marehemu baba yangu kuingia kwenye muziki kwa kuhudhuria mazoezi ya kundi lao." Anasema alianza muziki kwa kujifunza kupiga ala mbalimbali kabla yakujikita kwenye utunzi na uimbaji akiwa katika kundi hilo la African hadi baba yake alipohama na kuanzisha kundi lake binafsi la Coast Modern Taarab mwaka 1998 ambapo alizidi kubobea kwenye fani hiyo.

Tego anasema mwaka 2003, aliliacha kundi hilo la baba yake na kwenda Zanzibar kujiunga na kundi la JKU, lakini alilazimika kurejea jijini Dar es Salaam miaka miwili baada ya baba yake kufariki na baada ya mazishi alilazimika kubeba jukumu la kuliongoza kundi hilo. "Nilirejea Dar mwaka 2005 baada ya baba kufariki na nikabeba jukumu la kuliongoza kundi hilo ambapo tangu liwe chini yangu tumeachia albamu tatu tofauti, ya kwanza ikiwa ni I'm Crazy 4 U', 'Kupenda Isiwe Tabu' na 'Damu Nzito' ambayo inaendelea kutamba kwa sasa," anasema.

Tego anasema fani ya muziki imempa mafanikio mengi ikiwemo kujenga nyumba anayoishi na familia yake, kumiliki gari, kuwasomesha na kuwalisha wanae wanne pamoja na kumiliki miradi mingine ya kibiashara ambayo hakupenda yaanikwe gazetini. Mkali huyo, anayefananishwa na Mzee Yusuph wa Jahazi Modern, kwa namna ya madoido yake ya uimbaji, alisema hakuna kinachomuuma kama wizi wa kazi za wasanii unafanyika nchini, akidai kama angekutana na Rais wa Tanzania, hilo ndio lingekuwa kilio cha kwanza kwake.

"Ningemuomba Rais atusaidie kushughulikia wizi wa kazi zetu, tunaibiwa sana, licha ya kuwepo kwa COSOTA na asasi nyingine za kukomesha vitendo hivyo, ila kama mie ningekuwa Rais wa nchi ningepigana kuinua maisha ya wananchi pamoja na kuipa kipaumbele michezo na sanaa kwa sababu ni njia nzuri ya kutatua tatizo la ajira nchini," anasema Tego.

Tego, anayeshabikia klabu ya Yanga na Arsenal ya Uingereza, alisema hakuna tukio la furaha kwake kama kukubalika kwa kazi yake ya 'I'm Crazy For You', iliyoliinua Coast Modern na kuzalisha albamu iliyobeba jina hilo iliyomweka kwenye ramani ya muziki wa taarab nchini. Nyota huyo, aliyeoana na Fatuma Mohammed aliyezaa naye watoto wanne, Said , Ikram, Khairat na Ashura anapendelea wali kwa samaki na kinywaji anachopenda kukitumia baada ya chakula ni juisi.

Tego, mwenye ndoto za kuwa mwanamuziki wa kimataifa kwa kuitangaza taarab nje ya mipaka ya Afrika, alisema pamoja na kuimba taarab, anavutiwa sana na Jose Mara wa FM Academia na Christian Bella wa malaika bendi. Huyo ndie omary tego the special one ukipenda muite mgodi unaotembea mkurugenzi wa coast modern taarab yenye makazi yake jijini dar!.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni